|
Multithumb found errors on this page:
There was a problem loading image /homepages/30/d171144326/htdocs/www/cheza/html/images/stories/si_mchezo_62_cover.jpg
There was a problem loading image /homepages/30/d171144326/htdocs/www/cheza/html/images/stories/si_mchezo_62_cover.jpg
  If you are among those who think vocational training is for young people who have failed to find fulfilling income generating activities then you should make sure that you do not miss reading Si Mchezo 62. The issue has exciting stories that go way beyond vocational training issues as in the cover story which reminds us that there is no such a thing as male jobs. If you cannot read Swahili then get someone to translate for you! Read on...
 
 
 
Hakuna kazi ya kiume…
Nilipokuwa mdogo nilifikiria jinsi gani nitaweza kuwa na maisha mazuri yanayotokana na juhudi zangu. Wazo langu hilo sikulifumbia macho kwani nilipo sasa ni kama ndege kapenya ‘tunduni’ ingawa bado napambana hadi kieleweke.
Jina langu ni Samila Hamisi (28), nilimezaliwa Mpanda, Rukwa. Nimejaaliwa mtoto mmoja (3). Nilipata elimu ya msingi katika Shule ya Kashoto, Mpanda. Baadaye nikajiunga na Shule ya Sekondari Mwangaza ambako nilimaliza kidato cha nne mwaka 2000. Sikufaulu kuendelea na elimu ya juu ya sekondari hivyo ilinibidi kubaki nyumbani kwa mwaka mmoja.
Mwaka 2001, nilikuja Tabora kutafuta kazi. Nikapata kazi kwenye kampuni inayojishughulisha na ulinzi na kufanya usafi. Nilifanya kazi kwa miaka mitatu nikiishi kwa baba mdogo. Nilikuwa nikijinyima ili kuweka pesa kwa ajili ya kujilipia masomo. Haikuwa rahisi lakini nilijiwekea malengo.
Katika pitapita zangu nikiwa Tabora, nilikuwa natafuta namna ya kujiendeleza kimasomo nikiwa naziangalia fursa za kozi zenye soko katika mkoa huu. Nilipenda kazi ya ufundi umeme. Siku moja nikamuona dada Jennifer ambaye alikuwa akifanya kazi za ufundi umeme. Nilikuwa namuona kama mwanamke wa kipekee. Ilinibidi nimuulize huo ujuzi aliupata wapi? Aliniambia amesomea VETA. Kwa kuwa nilikuwa na ‘mshiko’ niliodunduliza, niliamua kujiunga na VETA kusomea kozi ya umeme. Nilimshirikisha baba mdogo lakini alihofia kuhusu masuala ya ada nilipomwondoa hofu hiyo aliniunga mkono.
Nikaanza kusoma huku nikifanya kazi. Ilikuwa shughuli pevu kuwajibika pande zote mbili. Wakati mwingine nilikatishwa tamaa na marafiki kuwa sitaweza kumaliza kusoma masomo magumu hivyo wakati nikifanya kazi, lakini nilishafanya uamuzi.
Baada ya miezi sita, nilimaliza daraja la tatu ambalo nilijifunza ufungaji wa umeme. Niliendelea hadi daraja la kwanza. Nilimaliza mwaka 2011. Niliomba kufanya mafunzo kazini kwenye Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO). Niliifurahia sana kazi hiyo ingawa nilikuwa nikikumbana na maswali mengi kutoka kwa wasichana wenzangu wakiniuliza kwa nini nafanya kazi za kiume. Jibu lilikuwa moja tu kuwa hakuna kazi inayobagua jinsia. Wengine walitamani kuwa kama mimi lakini wanahofia shinikizo rika.
Sasa ni fundi wa umeme ambaye navuma kwa kiasi changu. Nimefanikiwa kujitegemea na hata nimenunua kiwanja huko kwetu Mpanda ambako natarajia kukiendeleza.
Ndoto yangu ni kujiendeleza zaidi kielimu na pia kuwaendeleza wadogo zangu. Kuna wasichana ambao walikuwa wakinikatisha tamaa mwanzoni, sasa nimekuwa mshauri wa wengi. Ile kampuni niliyokuwa nikifanya kazi ya ulinzi na usafi ilishindwa kuendelea kwa kukosa mtaji hivyo wafanyakazi wengi waliachishwa kazi. Kwa kuwa nilijiendeleza, TANESCO waliamua kunipa kazi ambayo nafanya kwa mkataba. Wasichana wengi niliokuwa nafanya nao kwenye kampuni ile hawana kazi kwa sasa.
Nawashauri wasichana wajiendeleze kielimu bila kuchagua fani kwani mwanamke anaweza kufanya kazi yoyote mradi akijue na kukiendeleza kipaji chake.
Vilevile ni vizuri kuchukua tahadhari katika sehemu za kazi kama vile kuvaa vifaa vya kujikinga na hatari sehemu za kazi, kuepuka lugha zisizostahili kazini, n.k. Kwa uzoefu niliokutana nao sehemu za kazi, vipo vishawishi vinavyoweza kukufanya ujihusishe na ngono zembe na kupata maambukizi ya VVU.
Jichunge.
|
Follow us on: